Mafunzo Uandaaji Wasifu wa Kijamii, Kiuchumi Kuimarisha Mipango ya Maendeleo Nchini
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule amesema kuwa mafunzo ya uandaaji wa Wasifu wa kijamii na kiuchumi wa mikoa pamoja na Halmashauri yataisaidia Serikali kupata Takwimu rasmi ambazo zitatumika kupanga na kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo nchini.
Mhe. Senyamule ameyasema hayo, wakati akifunga mafunzo ya Uandaaji wa Wasifu wa Kijamii na Kiuchumi wa Mikoa na Halmashauri zote nchini, tukio ambalo limefanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma tarehe 14 Mei 2026.
Kiongozi huyo amesema wasifu wa kijamii na kiuchumi ni nyenzo muhimu kwa Serikali na wadau katika kufanya maamuzi sahihi ya kupanga matumizi ya rasilimali, kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo katika mikoa mbalimbali nchini.
“Takwimu zitakazokusanywa kupitia zoezi hili, zitasaidia kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano (FYDP IV 2026/27–2030/31) unaolenga kukuza uchumi jumuishi na kuongeza ajira”. Amesema Mhe. Senyamule na kuongeza;
“Serikali imewataka washiriki wa mafunzo hayo kuhakikisha wanatumia elimu waliyoipata kwa ufanisi katika ukusanyaji wa taarifa sahihi kwenye maeneo yao ya kazi ili kuwezesha upatikanaji wa takwimu rasmi zenye ubora.”
Pia, amewahimiza washiriki kushirikiana na taasisi za umma na binafsi katika ukusanyaji wa taarifa za kijamii na kiuchumi ili kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa na kuleta matokeo chanya kwa maendeleo ya Taifa.
“Nawaasa wamiliki wa taasisi na shughuli za kiuchumi za Serikali na binafsi kutoa ushirikiano kwa watakaokuja kukusanya taarifa.” Amesema Senyamule.
Aidha, Mkuu wa Mkoa huyo amewapongeza washiriki wa mafunzo hayo kwa kujituma na kueleza imani yake kuwa watatekeleza jukumu la ukusanyaji wa taarifa kwa weledi na kwa wakati.
Kadhalika, aliishukuru Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kuratibu mafunzo hayo kwa kuwa ndiyo taasisi pekee yenye jukumu la kukusanya, kuchakata na kusambaza Takwimu rasmi nchini, pamoja na wakurugenzi wa Halmashauri kwa kuwawezesha watumishi wao kushiriki katika mafunzo hayo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.