NBS, SADC Watoa Mafunzo ya Python kwa Wachakataji Takwimu
Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa kushirikiana na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), zinaendesha mafunzo ya uchakataji na uchambuzi wa Takwimu kwa kutumia Programu ya Python, yakihusisha wadau mbalimbali kutoka ndani ya Mfumo wa Taifa wa Takwimu (National Statistical System–NSS).
Washiriki wa mafunzo hayo ambayo yameanza tarehe 11 hadi tarehe 22 Mei 2026, kwenye Ukumbi wa Mikutano uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini Dodoma, wanatoka Benki Kuu ya Tanzania - BOT, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na wataalamu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu.
Akifungua mafunzo hayo, Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Dkt. Amina Msengwa, amesema ana matumaini kuwa mafunzo hayo yatawezesha kufanyika kwa uchambuzi wa kina wa Takwimu rasmi ambazo tayari zimeshazalishwa pamoja na zile zinazotarajiwa kuzalishwa siku zijazo.
Dkt. Msengwa amesema washiriki wa mafunzo hayo watakuwa chachu ya kusambaza ujuzi kwa wataalam wengine ambao hawajapata nafasi ya kushiriki, hatua itakayosaidia kupunguza gharama kwa Serikali za kuhitaji wataalam kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kutoa mafunzo hayo.
Kwa upande wake, Mtakwimu Mwandamizi kutoka NBS, Milimo Mashini, amesema mafunzo hayo yamelenga kuboresha na kuimarisha uchakataji na uchambuzi wa takwimu, kuongeza ufanisi katika utendaji kazi, pamoja na kuharakisha uchakataji na utoaji wa matokeo ya takwimu.
Amesema mafunzo hayo pia yatawezesha utengenezaji wa mifumo ya kiotomatiki ya programu itakayosaidia katika uchambuzi wa data na kuongeza ubora wa kazi za kitakwimu.
Aidha, Mashini ameishukuru Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwa kukubali kushiriki katika mafunzo hayo, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha ushirikiano mzuri uliopo kati ya NBS na SADC katika kuwajengea uwezo wataalam wa takwimu pamoja na kuunga mkono shughuli za uzalishaji wa Takwimu nchini.